Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam
imewateua majaji watatu kusikiliza maombi ya makampuni ya kuzalisha
umeme ya IPTL na PAP ya kutaka kuzuia utekelezaji wa maazimio ya
Bunge kuhusu kashfa ya akuanti ya Tegeta Escrow.
Maombi ya kesi hiyo ambayo yataanza
kusikilizwa kesho Jijini Dar es Salaam yatasimamiwa na majaji hao
watatu ambao ni Jaji kiongozi Augustine Mwarija, Jaji Gadi Mjemas
pamoja na Jaji Stela Mugasha.
Kwa mujibu wa hati ya kesi hiyo,
IPTL na PAP inadai kwamba kilichofanyika ndani ya Bunge ni kinyume
cha Katiba ya Jamhuri na kina lengo la kugombanisha mihimili mitatu
ya dola; yaani Bunge, Mahakama na Serikali.
Hati hiyo inadai kwamba maazimio ya
Bunge yanakiuka Ibara ya 13(1) ya Katiba ya Tanzania inayosema watu
wote ni sawa mbele ya sheria na wanastahili kutendewa haki bila
kubaguliwa.
Hati hiyo inadai kuwa maazimio ya
Bunge pia yamevunja Ibara ya 13(3) ya Katiba ya Tanzania inayotaka
haki za kila mtu zilindwe na kuamuriwa na Mahakama, ikiongeza pia
kuwa Bunge limekiuka kifungu cha 6(a) cha Ibara ya 13 ya Katiba
kinachosema kuwa kila mtu ana haki kusikilizwa na kukata rufaa au
kudai haki zake kisheria; pamoja na kifungu cha 6(b) cha ibara hiyo
kinachosema mtu atakuwa hana hatia hadi pale Mahakama itakapomkuta na
hatia.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni